Friday, March 2, 2012

SHULE INAPOJENGWA, KUSAJIRIWA NA KUPOKEA WANAFUNZI BILA VYOO

Na Renatha Kipaka

 BUKOBA.

 Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera, imeombwa kujenga vyoo katika shule ya msingi Kashabo, iliyanzishwa 2011 bila huduma hiyo, ili kunusuru afya za wanafunzi wanaosoma katika shule hiyo, ambao wanahangaika kufuata huduma ya choo shule jirani.

 Diwani wa kata Hamugembe iliko shule hiyo, Bwana Robert Katunzi alitoa ombi hilo katika kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo, kilichofanyika hivi karibuni.

Bwana Katunzi alisema kuwa shule hiyo yenye wanafunzi 164 ilianzishwa kwa lengo la kupunguza msongamano katika shule ya msingi Rwamishenye ambayo mwaka 2011 waliandikishwa watoto 200 na kulazimika kuhamisha watoto 80 kwenda katika shule hiyo mpya.

 Alisema kuwa, tangu imejengwa shule ya msingi Kashabo wanafunzi wake wanatumia vyoo vya shule jirani ya Rwamishenye, na kwamba sasa ifikie wakati watoto hao waonewe huruma, wajengewe vyoo ili wapate pa kujihifadhi, hasa ikizingatiwa kuwa wale ni watoto wadogo wa darasa la kwanza na la pili.

 Akizungumzia hoja hiyo mwenyekiti wa kamati ya mipango miji wa manispaa ya Bukoba, Bibi Mwajabu Galyatano ambaye ni diwani wa viti maalum alisema kikao cha kamati ya fedha kilichokaa hivi karibuni, kiliazimia kukamilisha viporo vya miradi vilivyopo, ili kupunguza malalamiko ya wananchi.

 Bibi Galyatano alisema kuwa sio mradi huo tu bali ipo na miradi mingine imesahaulika, na kuwashauri madiwani wenzake kupeleka taaarifa manispaa kuhusiana na viporo mbalimbali vya miradi ili vishughulikiwe.

Alisema kuwa kwa sasa hawataanza kutekeleza miradi mipya, mpaka fedha zipatikane kwa ajili ya kutekeleza viporo hivyo .

 Naye naibu meya wa manispaa hiyo Bwana Alexander Ngalinda aliiomba kamati inayohusika na ufuatiliaji wa viporo vya miradi, kupita mitaani na kuvianisha haraka, ili iweze kutoa vipaumbele.




Wanafunzi wa shule moja ya msingi hapa nchini wakijifunza chini ya miti  kutokana na uhaba wa vyumba vya madarasa (picha ya mtandao)

ulemavu sio kulemaa

 Vijana wenye ulemavu wakiwa katika shughuli zao za kila siku za kujitafutia riziki kwa kutengeneza vifaa mbalimbali vya kiasili ikiwamo ngoma, urembo na malimba, kupitia kikundi chao cha Bukoba Disabled Assistance Project (BUDAP) cha mjini Bukoba.
Mwenyekiti wa chama cha waandishi wa habari mkoani Kagera Bw. John Rwekanika akiangalia baadhi ya vifaa vya asili ikiwamo ngoma, wakati waandishi wa habari walioko katika mafunzo ya online journalism walipotembelea kituo chenye kumbukumbu za kale cha Bukoba Museum.